CUF Kuandamana Kupinga Marudio Ya Uchaguzi Zanzibar

CHAMA
 cha Wananchi (CUF) Bukoba kimejiandaa kufanya maandamano ya amani 
keshokutwa, kwa ajili ya kupinga kufanyika upya uchaguzi wa Zanzibar 
unaotarajiwa kuwa Machi mwaka huu.
Kimeiomba
 pia serikali ya awamu ya tano, kuchukua uamuzi wa kumtambua Maalim Seif
 Sharif Hamad kuwa ndiye mshindi wa uchaguzi wa urais Zanzibar na kuwa 
hakiko tayari kurudia uchaguzi huo tena.
Akizungumza
 na waandishi wa habari juu ya msimamo wa chama hicho, Kaimu Mwenyekiti 
wa chama hicho Saverina Mwijage, alisisitiza kuwa kamwe chama hicho 
hakitakuwa tayari kurudia uchaguzi huo uliotangazwa na Tume ya uchaguzi 
ya Zanzibar (ZEC) kuwa utafanyika Machi 20,kwa kile kinachodaiwa ni 
kufutwa uchaguzi wa Oktoba 25,mwaka jana.
“Tumedhamiria
 kuandamana ili kumfikishia ujumbe wetu Rais John Magufuli kupitia kwa 
Mkuu wa mkoa wa Kagera, John Mongella lengo letu hasa ni kupinga 
uchaguzi wa Zanzibar. Hali ya Zanzibar kwa sasa haiko shwari, watu 
wanatishiwa maisha yao, wanaishi kwa hofu juu ya maisha,” alisisitiza.
Mwijage
 ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake wa CUF Taifa, 
alisema chama hicho kinatambua uchaguzi ulishakwisha na tume hiyo 
ilishatoa vyeti kwa walioshinda, kwa mantiki hiyo CUF inamtambua Maalim 
Seif kuwa alishinda katika uchaguzi huo.
Alisema
 maandamano hayo yanatarajiwa kuanzia saa 4:00 asubuhi hadi saa 9:00 
alasiri na baadaye utakuwepo mkutano wa hadhara katika Uwanja wa 
Mashujaa Mayunga ulioko mjini Bukoba ili kuutangazia umma juu ya msimamo
 wa chama hicho na baada ya hapo watazunguka katika wilaya za Muleba, 
Missenyi na Karagwe.

0 comments: