Hii ni Vita Sasa !!!! Nape Aitaka Chadema Imtimue Lowassa

CCM
 imemjibu mwanasheria Mkuu wa Chadema ikisema ili chama hicho kikuu cha 
upinzani kionekane kinapambana na ufisadi kwa vitendo, kinatakiwa 
kumuunga mkono Rais John Magufuli na kumvua uanachama Waziri Mkuu wa 
zamani, Edward Lowassa.
Akizungumza
 na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, katibu wa itikadi na 
uenezi wa chama hicho tawala, Nape Nnauye alisema Chadema iliachana na 
ajenda ya kupambana na ufisadi baada ya kumpokea Lowassa  Julai mwaka 
jana baada ya jina lake kukatwa katika mchakato wa CCM kusaka mgombea 
wake wa urais.
“Sisi
 hatukumpitisha (Lowassa) awe mgombea wetu wa urais kwa sababu hiyo (ya 
ufisadi) na ndiyo maana yeye mwenyewe aliamua kuondoka na kwenda 
Chadema,” alisema Nape.
“Hata katika kampeni za uchaguzi mkuu, Chadema hawakuzungumzia ajenda ya ufisadi, ni kama Lowassa aliifunika tu.”
Alikuwa
 akimjibu Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu ambaye  juzi alisema 
ufisadi ni ajenda ya kudumu ya chama hicho kwa kuwa Rais Magufuli 
hataweza kuufumua wote katika kipindi cha miaka mitano.
Huku
 akichelea kueleza kiundani sababu za CCM kutomfukuza Lowassa kwa tuhuma
 za ufisadi mpaka alipoamua kujiondoa na kujiunga na Chadema, alisema 
kauli ya Lissu inalenga kuwahadaa Watanzania.
“Kauli
 ya Lissu ni ya kushangaza sana. Sisi tunajua jinsi ambavyo Chadema na 
washirika wake walivyojitenga na ajenda ya ufisadi. Kama kweli 
wanaupinga, basi wamuunge mkono Rais Magufuli ambaye kwa sasa anapambana
 na ufisadi kwa kasi,” alisema mbunge huyo wa Mchinga.
“Wakati
 mwingine kila jambo hufanyika kwa wakati wake. Suala la kupinga ufisadi
 CCM lilianza siku nyingi tangu enzi za kujivua gamba. Tumeendelea nalo 
mpaka watu wakajiondoa wenyewe,” alisema Nape.
Alisema
 hoja ya kupinga ufisadi ndani ya CCM ilikibeba chama hicho katika 
Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana na kikapata ushindi mnono, huku Chadema 
iliyokuwa ikilia na ufisadi ikishindwa.
 “CCM tulieleza sababu za kutompitisha Lowassa kugombea urais na hilo lilikuwa wazi,” alisema.
Katika
 ufafanuzi wake wa juzi, Lissu alisema ili apambane na ufisadi, Rais 
Magufuli anapaswa kuacha tabia za CCM na kumtaka mwenyekiti wa Tume ya 
Uchaguzi Zanzibar (ZEC) amtangaze mshindi halali wa Uchaguzi Mkuu ambao 
Chadema wanaamini Maalim Seif Sharif Hamad alishinda.
Pia
 Lissu alimtaka Rais ataje majina ya waliokwepa kodi ili kama 
watajitokeza kuwania uongozi, wadhibitiwe kwa kuwa Katiba imezungumza 
kwa maneno makali dhidi ya vitendo hivyo viovu.
Aidha,
 aliponda uteuzi wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter 
Muhongo anayetajwa kuhusiska katika sakata la uchotwaji wa Sh3060 
bilioni kutoka akaunti ya Tetega Escrow.
Miaka 39 ya CCM
Akizungumzia
 maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 39 ya kuzaliwa kwa CCM, Nnauye 
alisema uzinduzi utafanyika Januari 31, visiwani Zanzibar na mgeni rasmi
 atakuwa makamu mwenyekiti wa chama hicho na Rais wa Zanzibar, Dk Ali 
Mohammed Shein.
Alisema
 kilele cha maadhimisho hayo kitakuwa Februari 6, mjini Singida na 
yataongozwa na mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete ambaye aliiongoza 
Serikali ya Awamu ya Nne.
“Viongozi
 wa kitaifa na baadhi ya wajumbe wa Kamati Kuu watakaohudhuria 
maadhimisho haya watapangiwa shughuli za ujenzi wa chama na taifa katika
 wilaya zote za mkoa wa Singida, siku tatu kabla ya kilele cha 
maadhimisho,” alisema.
Alisema
 mikoa yote nchini inapaswa kuandaa shughuli hiyo wiki moja kabla ya 
maadhimisho, na kwamba lengo ni kufanya shughuli za ujenzi wa chama 
hicho katika maeneo yao.
“Tutakachokifanya
 wiki hiyo ni kupokea wanachama wapya, kufanya mikutano ya kuwashukuru 
wananchi kwa kuiamini CCM na kuichagua iendelee kuongoza, kuhamasisha 
wananchi kufanya kazi ili kujiletea maendeleo,” alisema.

0 comments: