Jaji Damian Lubuva Amtaka ' Lowassa' Aache Kuupotosha Umma

Mwenyekiti
 wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Jaji Damian Lubuva amewataka 
wanasiasa walioshindwa kwenye Uchaguzi Mkuu waache kujitangaza kuwa 
walishinda, akisema wanapotosha wananchi.
Kauli
 hiyo ya Jaji Lubuva imekuja siku chache baada ya aliyekuwa mgombea 
urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa kudai kuwa kama si matokeo 
kuchakachuliwa, alikuwa na nafasi kubwa ya kushinda kwa sababu wananchi 
walishaichoka CCM na wakawa wanataka mabadiliko.
Lowassa
 alisema hayo katika mahojiano maalum na waandishi wa habari ofisini 
kwake, akisema yeye na Ukawa walishinda kwa kishindo isipokuwa matokeo 
yalivurugwa makusudi ili CCM iendelee kubaki madarakani.
Jana,
 akiwa kwenye mkutano wa tathmini kati ya NEC na asasi za kiraia kuhusu 
utoaji elimu kwa mpigakura uliofanyika Dodoma, Jaji Lubuva alisema 
uchaguzi umeshapita na kilichobaki sasa ni kufanya kazi tu.
Bila
 ya kutaja jina la mwanasiasa huyo, Jaji Lubuva alisema kama kuna mtu 
alishindwa katika uchaguzi uliopita, ajipange kwa ajili ya uchaguzi mkuu
 ujao mwaka 2020.
“Hata wananchi wanawashangaa kwa kuwa wao ndio walioamua ni nani anafaa kuwaongoza,” alisema Jaji Lubuva.
Alisema
 kuwa NEC ilikuwa inapokea matokeo ya uchaguzi kutoka majimboni na 
kuyasoma kama yalivyotumwa na katika hilo hakuna wakala hata mmoja wa 
chama ambaye aliyapinga matokeo hayo.
“Sasa
 nashangaa kuna baadhi ya wagombea wanaotaka Tume ifukuzwe kazi eti tu 
kwa sababu wao hawakushinda. Naomba ifahamike kwamba katika kila 
uchaguzi duniani kuna kushinda na kushindwa.
"Sasa
 kama kila atakayeshindwa atataka tume ifukuzwe kazi hapatakuwa na tume 
ya uchaguzi kwa sababu kila atakayekuwa anashindwa atakuwa anataka tume 
ifukuzwe kazi,” alisema Jaji Lubuva.
Chadema,
 ambayo iliungana na vyama vitatu kuunda Ukawa, iliitaka NEC kusitisha 
utangazaji matokeo ikidai kuwa kilichokuwa kikitangazwa ni tofauti na 
takwimu walizokusanya kutoka majimboni. Lakini NEC ikaendelea kutangaza.
Baadaye,
 Chadema ililalamika ikidai kituo chao cha kukusanya na kujumlisha 
matokeo kilivamiwa na polisi na kompyuta kuchukuliwa na hivyo kuvuruga 
ufuatiliaji wao wa matokeo.
Kwa
 upande wake mkurugenzi wa huduma kutoka NEC, Emmanuel Kavishe alisema 
kuwa Tume inafanya kazi kwa mujibu wa sheria na Katiba na kwamba hata 
siku moja haijawahi kumpendelea au kumuonea mtu yeyote.
Katika uchaguzi wa urais, John Magufuli alipata kura milioni 8.8 huku Lowassa akipata milioni 6.07. 

0 comments: